0

  1. “MIAKA ya nyuma kabla hatujapata elimu ya usafi wa mazingira wengi walikuwa hawana vyoo na walikuwa wakijisaidia vichakani au porini”.
Ni maneno ya Julieta Saileni, mkazi wa Ugogoni Kongwa Mjini, mkoani Dodoma. Mwananchi huyo anasema, wakati huo ustaarabu wa kujisaidia chooni haukuwepo na kwamba, watu walikuwa wakijenga nyumba zisizo na vyoo. Julieta anasema sasa hali imebadilika, hakuna vyoo vya magunia eneo hilo. Kwa mujibu wa mwananchi huyo, mazoea ya kujisaidia vichakani na wakati mwingine karibu na vyanzo vya maji hayapo tena. Anasem

a kaya nyingi zina vyoo vilivyoboreshwa na vinavyotumika.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Ugogoni Sarah Kimonga anasema, kabla ya kutolewa kwa elimu chini ya Mradi wa Usafi wa Mazingira Tanzania (UMATA) kaya zilikuwa zikishirikiana vyoo kwa kuwa ujenzi wa vyoo haikuonekana kama ni jambo muhimu.

“Hali hiyo ilisababisha kinyesi kutapakaa kila mahali hasa porini. Tulikuwa tukiogopa hata kutembea kwenye majani,” anasema Kimonga. Anasema watu sasa wamestaarabika na mlipuko wa magonjwa haupo tena. Ofisa Afya Kata ya Ugogoni, Iqubal Janja anasema, wakati wa kampeni hiyo ikianza asilimia 80 ya wananchi hawakuwa na vyoo lakini kutokana na uhamasishaji watu wamebadilika na kuona umuhimu wa kaya kuwa na choo bora na kukitumia.

“Wengi walikuwa wakiishi kwa mazoea kwani alikuta mzazi wake akiwa hana choo na hivyo waliona hakuna umuhimu wa kuwa na choo,” anasema Janja. Mtendaji wa kijiji cha Ugogoni, Cecilia Bajuta anasema hali ilikuwa mbaya kwa kuwa wananchi wengi hawakuwa na vyoo na walipelekwa kwenye Baraza la Migogoro la Kata. Anasema, wananchi hao walilazimishwa kujenga vyoo na aliyeshindwa alilipa faini Sh 50,000 na kusimamiwa hadi alipokijenga.

Anasema jumla ya wananchi 13 tayari wamefikishwa katika baraza la migogoro na kuchukuliwa hatua na wote sasa wana vyoo. Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Bituni Msangi anasema kampeni ya UMATA ni ya kitaifa na inatekelezwa katika wilaya zote Tanzania.

“Wilaya yetu ya Kongwa ni moja kati ya wilaya tatu za mkoa wa Dodoma zikiwemo wilaya nyingine za Bahi na Chamwino zinazosimamiwa na shirika la kimataifa la Plan pamoja na mashirika mengine ya utekelezaji likiwemo SAWA ambao wamekuwa wakishirikiana nasi kuanzia ngazi ya wilaya, kata, vijiji na vitongojini katika kuhamasisha masuala ya afya na usafi wa mazingira,” anasema Msangi.

Mfuko wa Usafi wa Mazingira Duniani (GSF) umeona ni muhimu kusaidia jamii kuondokana na maradhi yatokanayo na ukosefu wa vyoo pamoja na kutonawa mikono kwa maji na sabuni. Msangi anasema, shirika la SAWA limekuwa likifanya uhamasishaji huo katika vijiji 23 katika kata saba za Ugogoni, Sejeli, Songambele, Mkoka, Matongoro, Makawa na Zoissa katika awamu ya kwanza kuanzia Septemba 2015.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo, hadi sasa Kijiji cha Ugogoni chenye vitongoji vitatu kimekuwa cha kwanza kumaliza kazi ya usafi wa mazingira hatua ya pili. Anasema, kabla ya mradi, wananchi wengi wa Wilaya ya Kongwa hawakuwa na vyoo; kwa tafsiri rahisi ni kuwa walikuwa wanajisaidia kwenye vyoo vya majirani vichakani na porini, hivyo kuchafua vyanzo vya maji na mazingira kwa ujumla. Uchafu huo ulisababisha magonjwa ya kuharisha, kipindu pindu na yale yanayotokana na maji machafu.
“Tunahitaji kuwa na mpango mkakati wa makusudi utakaotuwezesha kufikia hatua ya kwanza katika kipindi kifupi kijacho,” anasema Msangi. Anasema, kwa miezi kadhaa sasa Tanzania imekumbwa na ugonjwa wa kipindupindu. Takribani mikoa 18 imeripotiwa kuathiriwa na ugonjwa huo na kwamba, katika wilaya hiyo kipindupindu kimeathiri Tarafa ya Zoissa. Chanzo kikuu cha ugonjwa huo ni kula vyakula vilivyo na vimelea vya ugonjwa ambavyo hukaa kwenye kinyesi na husambazwa na nzi au kugusa, kushika kinyesi.
“Wagonjwa wengi wameripotiwa na baadhi ya ndugu zetu, Watanzania wenzetu wamepoteza maisha,” anasema Msangi. Anasema Serikali inatumia fedha nyingi kununua dawa na vifaa tiba ili kukabiliana na ugonjwa ambao wananchi wangeweza kuuzuia kwa kujenga vyoo na kuvitumia, kunawa mikono kwa sabuni na kutibu maji ya kunywa. “Fedha zinazotumika kutibu kipindupindu zingeweza kutumika kwenye miradi mingine ya maendeleo. Njia rahisi ya kuzuia kipindupindu ni kukata mawasiliano ya nzi na kinyesi au mtu kula kinyesi; hii ni pamoja na kuhakikisha hakuna nzi anayeingia na kutoka chooni” anasema Msangi.

Anataja njia nyingine ya kumaliza kipindupindu ni kuweka mfuniko kwenye tundu la choo muda wote, kumiminia dawa au majivu mara kwa mara ili kuondoa harufu ambayo ingeweza kumvutia nzi. Kusafisha tundu la choo ni safi, kuondoa mabaki ya kinyesi, na kusafisha eneo lililokuwa na kinyesi ni namna nyingine ya kukabili ugonjwa huo. Anataka viongozi na watendaji wa Serikali kila ngazi wamepewa maagizo kuhusu namna ya kulisimamia hilo na kutaka kila mwananchi awe mstari wa mbele kuitikia mwito wa kuutokomeza ugonjwa huo.

Msangi akitaka vijiji vingine wilayani huo kuiga yaliyofanywa Ugogoni ili kuondokana na aibu ya kujisaidia hovyo vichakan. Mmoja wa wafanyakazi wa Shirika la SAWA, Asnat Charles anasema, katika mradi huo wa usafi wa mazingira shirika hilo linahamasisha ujenzi na matumizi ya vyoo bora na mabadiliko ya tabia katika jamii na shuleni.

Anasema, SAWA wanatumia mbinu ya kushirikisha jamii kuhusu usafi wa mazingira kwa kutumia mbinu iitwayo CLTS (Community Led Total Sanitation) na miongozo ya taifa ya maji, afya na usafi wa mazingira katika wilaya ya Kongwa. Mradi huo pia unatoa elimu ya afya na usafi wa mazingira kwa shule za msingi ikimlenga mtoto ambaye ndiye chachu ya mabadiliko kwa mtoto mwenzake, ngazi ya familia na jamii kwa ujumla.

Anasema katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi wa UMATA shirika la SAWA kuanzia mwishoni wa Septemba mwaka 2015 linafanya kazi katika kata saba za Ugogoni, Sejeli, Songambele, Mkoka, Zoissa, Matongoro na Makawa “Mpaka sasa tumefanikiwa kufanya uhamasishaji wa matumizi sahihi ya vyoo, ujenzi wa vyoo na usafi wa mazingira kwa ujumla kwa kupitia mikutano ya hadhara, kutoa mafunzo ya afya na usafi wa mazingira kwa wahudumu wa afya 332, viongozi ambao ni watendaji kata saba vijiji 23, Vitongoji 83, waratibu wa elimu kata saba na walimu 44 katika shule 22 za msingi,” anasema Charles.

Anasema, kutokana na muongozo wa Wizara ya Afya, ili kijiji au kitongoji kifikie hatua ya pili ya uboreshaji wa masuala ya usafi wa mazingira inahitajika kuwa na vigezo kikiwemo cha kila kaya kuwa na choo kinachotumika na kifaa cha kunawa mikono yaani asilimia 100 ya vyoo kwa jamii na vifaa vya kunawa mikono. Taasisi zilizomo katika jamii zinapaswa kuwa na vyoo bora na vifaa vya kunawa mikono, na kutokuwepo kwa dalili za uzagaaji ovyo wa kinyesi katika mazingira yakiwemo makorongo, karibu na vyanzo vya maji na viwanja vya wazi katika jamii husika.

Anasema hadi sasa vitongoji vingi vilivyopo chini ya shirika la SAWA vipo katika hali nzuri ya kuacha kujisaidia ovyo kwani vipo kwenye hatua zaidi ya asilimia 75 ya utekelezaji wa mradi. “Hii ni hatua nzuri ukilinganisha na hali ilivyokuwepo mwanzo kabla ya utekelezaji wa mradi. Hatua hii imechangiwa sana na ufuatiliaji wa mara kwa mara katika ngazi ya kaya ili kuhakikisha wale watu ambao hawana vyoo wanajenga na pia kuhimiza umuhimu na faida za kunawa mikono kwa maji yanayotiririka hasa kwa kutumia teknolojia rahisi ya kibuyu chirizi,” anasema Charles.

Post a Comment

 
Top